Bismillahi naanza, kwa jina lake manani,
Hakika yeye wa kwanza, alotuletea dini,
Adam alimfunza, apokuja duniani,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Dini imetuhimiza, tuwepo msikitini,
Sote tuwe tunaweza, kuwa pamoja jamani,
Hilo tunalitimiza, bila ya shaka yakini,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Uzuri wa mila zetu, tunafanana na dini,
hatuwachi mila zetu, tukafata za ugeni,
toka enzi babu zetu, walokuwa vijijini,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Twaweka chakula chetu, hapo nje uwanjani,
Tunakula na wenzetu, kwa pamoja mkekani,
Kwenye masinia yetu, wala sio sahanini,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Anayepita njiani, wakati wa kufuturu,
Akaribishwa jamvini, aketi na kufuturu,
Huo wema kwa mgeni, naye huwa ashukuru,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Watu huwa furahani, wanapokuwa pamoja,
Vicheko vimdomoni, wala huulizwi hoja,
Pamoja na majirani, wote wawezao kuja,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Tudumishe mila zetu, tusiache abadani,
Tuthamini yalo yetu, tusifate ya wageni,
Ndio umuhimu kwetu, tuyapende kwa moyoni,
Ramadhani twafuturu, kwa pamoja uwanjani.
Illustration by Mosab Zkaria